Home » » WATUMISHI WAONYWA KUHUSU VIRIBA TUMBO‏

WATUMISHI WAONYWA KUHUSU VIRIBA TUMBO‏


 Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Dkt. Anselm Tarimo akizungumza na watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kabla ya zoezi la upimaji wa hiari wa magonjwa sugu yasiyoambukizwa pamoja na VVU katika ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wiki hii
Baadhi ya watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Shinyanga wakimsikiliza kwa makini Katibu Tawala wa Mkoa wakati wa zoezi la uhamasishaji na upimaji wa VVU pamoja na magonjwa sugu yasiyoambukizwa

Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya Afya Dkt. Ntuli Kapologwe akiwahamasisha watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kupima afya zao, mapema wiki hii katika zoezi hilo

 Dkt Sostenes Magezi kutoka Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga akiwaelimisha watumishi na kuwahamasisha kuhusu magonjwa sugu na yasiyoambukiza na kuwasihi kupima afya zao
Baadhi ya wakuu wa idara mbalimbali ofisi ya Mkuu wa Mkoa walioongoza zoezil hilo la kupima 
 Baadhi ya watumishi wakisubiri pia kupima afya zao katika hospitali ya Mkoa wa Shinyanga mara baada ya uhamasishaji
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Dkt Anselm Tarimo amewaasa watumishi kujenga tabia ya kufanya mazoezi ili kujiepusha na magonjwa sugu yanayotokana na ongezeko la mafuta mwilini.

Dkt Tarimo ametoa onyo hilo katika zoezi la uelimishaji, uhamasishaji na upimaji wa hiari wa ugonjwa wa UKIMWI na magonjwa sugu yasiyoambukizwa lilifanyika katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa na badae upimaji ulioendeshwa kwenye hospitali ya mkoa wa Shinyanga mapema wiki hii.

Amesema magonjwa hayo sugu ambayo ni shinikizo la damu, kisukari, saratani yamekuwa ni tatizo hasa kwa watumishi wengi kutokana na mfumo wa maisha ya sasa na kutofanya mazoezi na hivyo kuwa na vitambi (viriba tumbo) kwa sababu ya mafuta kuganda mwilini.
Tarimo amewataka watumishi kutosubiri kutengewa sehemu maalum au uwanja bali wajibidishe wenyewe kwani mazoezi yanaweza kufanyika popote hata maeneo ya nyumbani wanapoishi.

Naye mganga mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt Ntuli Kapologwe amewaeleza watumishi kuwa, kupima afya ni jambo muhimu sana kwani linaongeza matumaini ya kuishi mara taru zaidi ya mtu asiyeijua hali yake ya afya.

Awali, wataalam wa magonjwa hayo waliotoa elimu kwa watumishi,Dkt Sostenes Magezi na Bi. Ruth Kanoni wamesema mkoa wa Shinyanga ni moja ya mikoa yenye tatizo la magonjwa hayo sugu kutokana na watu kutoelewa umuhimu wa lishe bora na kufanya mazoezi, pamoja na kasumba ya kuona wenye vitambi ndio watu wenye afya njema.

Aidha, wameongeza kuwa ugonjwa wa UKIMWI bado ni tishio kwa mkoa wa Shinyanga ambapo kwa sasa maambukizi ya mkoa ni asilimia 7.4 juu ya ile ya kitaifa ambayo ni 5.1, hivyo wananchi wote wana wajibu wa kujilinda na kupima ili kujua hali ya afya zao.

Katika zoezi hilo ambalo litaendelea hadi kesho tarehe 27/11/2014 katika hospitali ya Mkoa wa Shinyanga, Katibu Tawala wa Mkoa amewaongoza watumishi wote kupima afya zao.


Na Magdalena Nkulu
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa 
Shinyang
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa