Home » » URASIMISHAJI WA BIASHARA NI MUHIMU(2)

URASIMISHAJI WA BIASHARA NI MUHIMU(2)

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Binadamu anapozaliwa hupewa jina ambalo humtambulisha au humtofautisha na binadamu wenzingine. Hata hivyo kutokana na mabadiliko ya sayansi, teknolojia na kijamii baadhi ya watoto hupewa majina hata wangali tumboni mwa mama zao!
Hali hii nayo hujitokeza katika biashara, kila mfanyabiashara angependa kuipa biashara yake jina ambalo lingeitofautisha na biashara nyingine kwa wateja wake.
Biashara kupewa jina ni moja ya hatua ya awali ya kurasimisha biashara husika kwani mwenye biashara atahitajika tena kupata cheti cha biashara na namba ya mlipa kodi kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania.
Hatua nyingine ni kupata leseni ya biashara kutoka katika manispaa au halmashauri husika na kufuata taratibu nyingine ambazo zimewekwa na mamlaka husika katika eneo lake la kufanyia biashara.
Urasimishaji biashara ni hali ya kuifanya biashara kutambulika kisheria kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizopo.
Kimsingi, jina la biashara kwa mtu binafsi husajiriwa baada ya kuanza kufanya biashara na huwa inashauriwa kusajiri jina la biashara angalau ndani ya siku 28 tangu kuanza kufanya biashara, mbali na hapo mwenye biashara atahitajika kutoa sababu za kutosajiri jina la biashara ndani ya siku hizo, ingawa pia baadhi yao hurasimisha biashara zao kabla ya kuanza kutegemeana na utashi wa mwenye biashara.
Katika nchi yetu na nyingine nyingi zinazoendelea, wajasiriamali wengi wadogo na wa kati wamekuwa wakifanya shughuli zao bila kuzirasimisha kutokana na sababu mbalimbali zikiwamo kushindwa kwa Serikali kuwa na mfumo mzuri pamoja na vivutio ambavyo vingewafanya wajasiriamali hao kurasimisha biashara zao.
Sababu nyingine ni wajasiriamali kutoona umuhimu wa kurasimisha biashara zao, na gharama kubwa za mchakato wa urasimishaji biashara kama vile muda na fedha. Matokeo ya kutorasimisha biashara kwa mjasiriamali ni kutotambulika kisheria na hivyo kuishi kama digidigi ndani ya mbwa mwitu.
Mara nyingi kumekuwa kukijitokeza ugomvi kati ya askari wa majiji/miji mbalimbali hapa nchini kwa madai kuwa wajasiriamali walio wengi wanafanyia biashara zao katika maeneo yasiyo rasmi jambo linaloashiria kuwa wajasiriamali hao wanafanya biashara ambazo hazitambuliki kisheria.
Ugomvi huo umekuwa ukisababisha wajasiriamali hao kupoteza mali zao walizochuma kwa shida, na imekuwa ikisababisha wengine kupelekwa mahakamani na kuhukumiwa ama kifungo gerezani au kulipa faini huku baadhi yao wakikata tamaa ya maisha na kurudi katika hali zao za awali za kutokuwa na kazi.
Vilevile imekuwa ikiwawia vigumu kupata misaada ikiwa ni pamoja na mikopo kutoka katika taasisi au watu mbalimbali kutokana na kutokuwa na uthibitisho wa kufanya biashara kama vile mahali maalumu wanapofanyia biashara, leseni za biashara na mambo mengine yanayoendana na masuala ya biashara zilizo rasmi. Wajasiriamali hawa wadogo wamekuwa hawana mchango wa moja kwa moja katika pato la taifa kwa sababu hawalipi kodi kwa mujibu wa sheria, ikiwa ni pamoja na kuwafanya wasikue kibiashara kwa kuogopa kulipa kodi kutokana na mazoea ya kufanya biashara zisizo rasmi kwa muda mrefu.
Kwa kuwa dunia ya sasa imekaa kama kijiji na ili ufanikiwa sharti hujitahidi kupambana ili ufahamike katika “kijiji hiki” urasimishaji wa biashara kwa wajasiriamali ni muhimu sana kwani mbali ya kuweza kupata tenda mbalimbali zinazotangazwa, na kupata habari za biashara kutoka vyanzo vya Serikali, kunakuwa na uwezekano wa kupata udhamini wa kuonesha na kuuza bidhaa katika maonesho tofauti.
Mwandishi wa makala haya ni mtaalamu wa Ujasiriamali na mtunzi wa vitabu
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa