Home » » Bodi ya Ithibati ya Wanahabari haitazuia uhuru wa habari

Bodi ya Ithibati ya Wanahabari haitazuia uhuru wa habari

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Benjamin Sawe
Maelezo
Wanadamu wameumbwa kwa hulka na silika ya kuwa na uwezo wa kuwasiliana miongoni mwao, jamii wanamoishi, taifa na hata ulimwenguni ili waweze kutimiza nia na azma yao ya kuwasiliana.
Ili mawasiliano hayo yakamilike ni lazima yabebe ujumbe unaokusudiwa kufikishwa katika jamii.
Ujumbe huo ili uweze kumfikia mlengwa, ni lazima iwepo njia ya kuufikisha ujumbe huo kwa mlengwa ambao huwasilishwa kwa maandishi (magazeti), sauti (redio) na picha (TV) pamoja na mitandao ya kijamii kupitia huduma ya inteneti.
Vyombo hivyo vya habari vinahusisha wataalamu ambao kazi yao ni kuhakikisha jamii inapata ujumbe kwa wakati ili kuweza kujenga, kuboresha na kuimarisha maisha yao kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni.
Vyombo vya habari hakika vimekuwa ndio macho na masikio ya wananchi ili kufikisha ujumbe unaohusu mambo mbalimbali yanayofanyika ndani na nje ya nchi.
Uanzishwaji wa Bodi ya Ithibati ya Wanahabari kama ilivyoainishwa katika Muswada wa Huduma za Habari wa mwaka 2016 hautaminya uhuru wa kutafuta na kusambaza habari.

Msingi wa haki ya kutafuta taarifa na kusambaza habari unatokana ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivyo watu wasiwe na hofu ya kuwa Bodi hiyo itawaminya watu kutoa mawazo yao.

Bodi ya Ithibati ya Wanahabari haiwezi kuwa kizuizi cha watu kutafuta na kusambaza habari kwani haki hiyo ipo kikatiba kupitia ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Sioni sababu yoyote ya kupinga uanzishwaji wake kwa kuwa malengo yake ni kuhakikisha inasimamia kanuni za maadili ya wanahabari hapa nchini na kuijengea heshima tasnia.

Pamoja na kuanzishwa kwa Bodi hiyo hakuna maana kwamba uanzishwaji wake utachukua majukumu ya taasisi zingine za habari zilizopo na kuongeza kuwa waandishi wa habari duniani kote wanafanya kazi kwa kufuata miiko ya maadili ya uandishi wa habari.

Suala kubwa kwa mwanahabari ni kuzingatia maadili na weledi wa taaluma yake ili kutekeleza majukumu yake pasipo kusababisha usumbufu kwa mtu au kikundi kingine

Muswada huu umeandaliwa kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo katika tasnia ya habari nchini ambazo ni pamoja na upungufu wa sheria zinazosimamia tasnia hii na mabadiliko ya teknolojia ya habari.
Changamoto ya kutokuwepo kwa udhibiti mzuri na usimamizi madhubuti ya viwango kwenye taaluma ya habari na utangazaji kumechangia madhila kwa jamii ikiwemo kuandikwa habari za upotoshaji, zinazokiuka maadili na zinazoweza kusababisha chuki, machafuko na uvunjifu wa amani.
Kutokana na mwingiliano wa teknolojia, mwaka 2003 serikali iliona umuhimu wa kuunganisha vyombo viwili; Tume ya Mawasiliano na Tume ya Utangazaji ili kuleta ufanisi wa usimamizi wa sekta na utoaji wa huduma bora kwa walaji.
Kwa ujumla sekta hii changamoto kubwa ni taaluma ya habari kutotambulika kama taaluma kamili inayopaswa kuheshimiwa, kukosekana vyombo madhubuti na huru vya usimamizi na badala yake mambo mengi kuwa chini ya serikali moja kwa moja
Sheria hii inaleta mageuzi makubwa katika usimamizi wa sekta ya habari hapa nchini ni sheria ambayo inakwenda kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu, kuifanya rasmi sekta ya habari kuwa sekta rasmi.
Wengi wamekuwa waathirika wa uandishi usiozingatia maadili na weledi wa taaluma ya habari na utangazaji kwa kukashifiwa au kuzushiwa taarifa zisizokuwa na ukweli wowote.
Mapendekezo yaliyomo katika sheria ya habari kwa kiasi kikubwa yamelenga kutatua changamoto ya kuwa na wanahabari waliosomea kazi yao na ambao wamewekeana maadili ya kufuata.
Ni sheria itakayoleta mifumo ya kisasa ya usimamizi na ni mifumo ambayo inaweza kugusa au kubadili namna tutakavyotenda na tunavyofikiria sasa,
Niwaombe wanatasnia wenzangu tuwe tayari kwa mabadiliko ili taaluma yetu iheshimiwe na sisi wenyewe tuheshimike zaidi.

Mwisho

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa