Home » » MAJAMBAZI 5 WA KIBITI WAUAWA KAHAMA

MAJAMBAZI 5 WA KIBITI WAUAWA KAHAMA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Imeandikwa na Raymond Mihayo, Kahama
MAJAMBAZI watano waliohusika katika mauaji katika maeneo ya Kibiti na Mkuranga mkoaniPwani, wameuawa kwa kupigwa risasi na Jeshi la Polisi wilayani Kahama mkoani Shinyanga walipokuwa wakitaka kufanya jaribio la kuwapora wafanyabiashara wa dhahabu wakijibizana risasi na Polisi.
Watu hao wameuawa juzi eneo la Mwanva, Kata ya Nyahanga mjini hapa baada ya majibishano ya risasi baina yao na askari Polisi wa doria waliokuwa zamu katika eneo hilo. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Simon Haule alisema hayo katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Kahama, Shinyanga ambako miili yao imehifadhiwa kusubiri kutambuliwa na ndugu zao.
Kamanda Haule alisema mauaji hayo yametokea saa 3.00 usiku baada ya jeshi hilo Kitengo cha Intelejensia kupata taarifa ya kuwa kuna majambazi ambao walikuwa wamejipanga kuvamia wafanyabiashara wenye maduka pamoja na wale wanaojihusisha na ununuzi wa madini ya dhahabu.
Alieleza baada ya Polisi kupata taarifa hizo, askari walienda katika eneo hilo ambalo lilikuwa na vichaka pamoja na mapango ambayo yalisababishwa na uchimbaji holela wa mchanga na walipofika walianza kurushiana risasi kabla ya kuwazidi na kuwakamata majambazi hao wakiwa wamejeruhiwa vibaya. Alisema majambazi hao walijeruhiwa vibaya na wakati wakipelekwa Hospitali ya Halmashauri ya Mji, wote watano walipoteza maisha.
Alisema baada ya kuuawa na kupekuliwa, walikutwa na bunduki moja aina ya Short Machine Gun (SMG) yenye risasi 25 pamoja na mabomu mawili ya kurushwa kwa mkono. Aliwaomba wananchi kuhakikisha wanashirikiana na Polisi kutoa taarifa nzuri kama hizo ili kuwabaini wahalifu waliopo katika jamii inayowazunguka na kuongeza suala la uhalifu ni la mtandao mkubwa.
Alisema jeshi hilo kwa sasa limejipanga kikamilifu katika kukabiliana na masuala ya uhalifu na kuongeza kuwa kama kuna watu wanahusika na uhalifu ni bora wakajisalimisha pamoja na zana walizonazo. Aliwataka ndugu wote ambao wanahisi hawajaonana na watu wao wa karibu kujitokeza kutambua miili ya watu hao kwani mpaka sasa hawajulikani ni wenyeji wa wapi nchini, hali ambayo inaweza kufanya miili kukaa muda mrefu katika eneo hilo la kuhifadhia maiti.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa