Home » » Kishapu kutumia mil.91/- kubadilisha uchumi

Kishapu kutumia mil.91/- kubadilisha uchumi

HALMASHAURI ya Wilaya ya Kishapu Mkoa wa Shinyanga imepanga kutumia kiasi cha sh.91,200,000 kwa ajili ya utekelezaji mpango kabambe wa kusaidia kubadilisha uchumi na hali ya maisha ya wafugaji katika wilaya hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa wiki iliyopita na Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Wilson Nkhambaku kwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi nchini, Dkt. Titus Kamani miongoni mwa shughuli zitakazotekelezwa kupitia fedha hizo ni ununuzi wa madume bora ya ng'ombe aina ya Mpwapwa na Borani.
Nkhambaku alisema wilaya imechukua hatua hiyo baada ya kubaini kuwepo kwa ongezeko la mifugo isiyo ya tija ya kutosha ambayo haiwezi kuwasaidia wafugaji kubadilisha hali za maisha yao na kuwaongezea kipato cha kutosha.
"Tayari suala la uboreshaji wa mifugo kwa kutumia madume bora limeonekana kupokewa kwa mwitikio mkubwa na wafugaji katika wilaya yetu ambapo kwa mwaka 2012 wilaya kwa kushirikiana na wafugaji iliweza kuhimilisha ng'ombe 200 katika vijiji vinne,"
"Vijiji hivyo ni pamoja na Mwamalasa, Somagedi, Songwa na Migunga ambako wafugaji walifanikiwa kupata ndama 15 sawa na asilimia 7.5 ya lengo tulilokuwa tumekusudia, lakini pia kwa mwaka 2012/2013 wilaya iliweza kununua madume bora 18 na kuyasambaza kwa wafugaji katika vijiji vitano," alieleza Nkhambaku.
Akifafanua mkuu huyo wa wilaya alisema katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 wilaya imetenga jumla ya shilingi 16,200,000 kwa ajili ya ununuzi wa madume bora 18 na mwaka 2014/2015 jumla ya shilingi 71,000,000 zitatumika kununulia madume bora 100 aina ya Mpwapwa na Borani yatakayosambazwa kwa wafugaji.
Nkhambaku alisema kiasi cha sh.4,000,000 kimetengwa kwa ajili ya shughuli ya uhamilishaji na kwamba matarajio ya wilaya hiyo ni kuendelea kushirikiana na wafugaji ili waweze kufuga kitaalamu na hivyo kuongeza tija katika mifugo yao.
Kwa upande wake Dkt.Kamani aliupongeza uongozi wa Wilaya ya Kishapu kwa jinsi ulivyoonesha ushirikiano katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo ikiwemo suala la kuwasaidia wafugaji waweze kupata mifugo bora itakayokuwa na thamani kubwa katika masoko.
"Ninakupongezeni kwa ushirikiano niliouona, hali hii itawasaidia zaidi wananchi wetu katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika maeneo yao, hili suala la kuwasaidia wafugaji wetu waweze kufuga kitaalamu na kuwa mifugo bora ni moja ya vipaumbele vyangu tangu nilipokabidhiwa wizara hii,"
"Ni aibu kuona zaidi ya miaka 50 ya uhuru wafugaji bado wanachunga ovyo, hawafugi kitaalamu, lazima tuwasaidie kwa kuwapa elimu ya kutosha ili wanufaike na ufugaji wao, na itapunguza kwa kiasi kikubwa migogoro iliyopo hivi sasa kati yao na wakulima, tuwatengee maeneo rasmi kwa ajili ya ufugaji tu," alisema Dkt. Kamani.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa