Home » » KISHAPU KINARA KWA UUZAJI PAMBA CHAFU

KISHAPU KINARA KWA UUZAJI PAMBA CHAFU

 Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, mkoani Shinyanga imetajwa kuongoza kwa kuuza pamba chafu iliyowekwa mchanga inayofikia tani 10, kitendo kinachoelezwa kufanywa na baadhi ya watu wasio waadilifu.
Akizungumza kwenye mkutano mkuu wa Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Shinyanga (Shirecu) juzi, Mwenyekiti wa chama hicho, Robert Jongela aliwataka wana ushirika kujiepusha na udanganyifu akisema unaathiri mapato na sifa ya ushirika kwa wanunuzi wa nje kuharibu mitambo.
Jongela alisema kuwa kitendo hicho kinaweza kuharibu sifa ya ushirika huo kimataifa kutokana na watu wachache wasio waadilifu, huku akibainisha kuwa kwa kipindi kirefu walikuwa hawajapata tatizo la kuuza pamba chafu.
“Hili tatizo limeibuka msimu huu wa mwaka 2014/15, baadhi ya vyama vimeuza pamba chafu iliyowekwa mchanga kwa makusudi. Tatizo hili limeikumba Wilaya ya Kishapu ambayo ndiyo inaongoza, mchanga kwenye pamba uliokutwa unafikia tani 10. Ni hatari, lazima tukemee hali hii,” alisema Jongela.
Mwenyekiti huyo alitoa onyo kwa viongozi wa vyama vya ushirika vya msingi na watendaji wao kuwa, wasipozuia hali hiyo inayoonyesha kuota mizizi watachukuliwa hatua kwani mkopo wanaopata benki unatozwa riba kubwa.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Annarose Nyamubi alisema kuwa Serikali itaendelea kusimamia ushirika kuhakikisha hauvunjwi wala kuingiliwa na mtu yeyote akieleza kuwa vyama vingi vimekufa kwa kukosa usimamizi imara.
Nyamubi aliutaka ushirika huo kuanzisha kilimo cha biashara za mazao mengine, ikiwamo alizeti ili kujikwamua zaidi kiuchumi badala ya kutegemea zao moja kwani hivi sasa kumekuwa na uhitaji mkubwa wa alizeti kwenye viwanda vya Wachina vilivyojengwa Shinyanga.
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa