Home » » WACHIMBAJI WA MADINI WAASWA

WACHIMBAJI WA MADINI WAASWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

WACHIMBAJI  wadogo wa madini nchini wametakiwa kuendelea kuifanya sekta hiyo kuwa ya heshima zaidi tofauti na miaka ya nyuma ambapo ilionekana kuwa ni sehemu ya watu waliokata tamaa.
Hayo yamesemwa mjini Mpanda na Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Rafael Muhuga wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa wachimbaji madini wadogo watakaonufaika na ambao hawatanufaika na Ruzuku ya Awamu ya Tatu ikiwa ni maandalizi ya kuwajengea uwezo ili ruzuku hizo zitumike kama ilivyokusudiwa kabla ya kukabidhiwa rasmi leo.
Alisema serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ruzuku itakayowawezesha wachimbaji hao kununua vifaa vitakavyosaidia kwenye shughuli za uchimbaji na kueleza kuwa, imedhamiria kuendelea kufanyia kazi changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ndogo ya madini nchini.
Alisema juhudi za serikali kuunga mkono shughuli za uchimbaji zinaonekana wazi na kuzitaja baadhi kuwa ni pamoja na kutoa ruzuku inayowezesha kupatikana kwa vifaa vya kisasa vya uchimbaji na uchenjuaji madini, uanzishwaji wa vituo vya mfano vitakavyotoa mafunzo ya teknolojia mbadala wa matumizi ya zebaki kwa wachimbaji wadogo wa madini na kuboresha na kurahisisha utoaji wa leseni ndogo za madini ambapo hivi sasa zinatolewa mikoani badala ya Dar es Salaam pekee.
Awali, akizungumzia Ruzuku ya Awamu ya Tatu, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini anayeshughulikia Madini, Profesa James Mdoe alisema katika awamu mbili zilizopita serikali imeona baadhi ya wanufaika wa ruzuku hizo wakifanya vizuri katika shughuli za uchimbaji na hata takwimu za uzalishaji madini zimeanza kuongezeka.
Aliongeza kuwa katika awamu mbili zilizopita, zipo kasoro ambazo serikali ilizibaini hivyo awamu ya tatu itatumika kuboresha kasoro hizo na kuongeza kuwa, katika awamu ya tatu sehemu kubwa ya fedha zitatumika katika kununulia vifaa ambavyo wazabuni watavisafirisha hadi katika eneo la kazi na kuwapa mafunzo wanufaika ya namna ya kuvitumia na pia mzabuni atatakiwa kutoa uhakikisho wa vifaa hivyo.
“Fedha zitapita Benki ya Maendeleo ya TIB, lakini Wizara ya Nishati na Madini itasimamia mchakato wote, hadi vifaa kufikishwa eneo la kazi na mnufaika kukabidhiwa. Vikundi vitakavyopaa ruzuku hii tutavisimamia kuhakikisha kinakuwa na katiba za vikundi vyao na uongozi imara,” alisisitiza.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa