Home » » DIWANI ALIYEDHALILISHWA KUMSHITAKI DC

DIWANI ALIYEDHALILISHWA KUMSHITAKI DC

na Ali Lityawi, Kahama
SAKATA la Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya, kumkwida na kumuondoa kwenye foleni ya chakula Diwani wa Nyihogo, Amos Sipemba (CHADEMA), limeingia katika sura mpya baada ya diwani huyo kudhamiria kulifikisha suala hilo katika vyombo vya sheria.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Diwani huyo alisema anadhamiria kuchukua hatua hizo dhidi ya mkuu huyo wa wilaya kutokana na kumvunjia heshima mbele ya kadamnasi na kwamba alitegemea baada ya Mpesya kutambua kosa lake angelimuomba radhi, lakini hilo halikutokea.
Alisema hakutarajia siku hiyo kama angekumbana na kadhia hiyo kutoka kwa kiongozi ambaye ofisi yake ilimuandikia barua ya kumuomba kujumuika katika ziara ya waziri mkuu kumuondoa pasipo kutumia ustaarabu kwenye mstari wa kwenda kupata chakula cha mchana kwa madai kuwa amekiuka utaratibu.
Aidha, alibainisha kitendo hicho ambacho kimewadhalilisha pia wapigakura wake tayari amelifikisha katika chama chake kwa ajili ya ushauri zaidi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Mpesya, alisema alichukua uamuzi huo kutokana na diwani huyo kuvunja utaratibu wa kwenda kuchukua chakula.
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa CHADEMA Wilaya ya Kahama, Juma Ntahimpera, amesema chama hicho kinatarajia kufanya harambee kubwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya wilaya itakayofanyika Septemba 30 mwaka huu katika Kata ya Bulyanhulu.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa