Home » » LEMBELI AMPONGEZA MGEJA KUTEULIWA

LEMBELI AMPONGEZA MGEJA KUTEULIWA



Na Antony Sollo, Kahama

HATIMAYE aliyekuwa mmoja wa waombaji wa nafasi ya uenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, James Lembeli, amempongeza mgombea wa nafasi hiyo mkoani hapa, Hamis Mgeja, kwa kuteuliwa kwake kutetea nafasi hiyo.

Lembeli aliyasema hayo jana mjini Kahama, katika mkutano wa uchaguzi wa viongozi wa ngazi mbalimbali unaoendelea ndani ya chama hicho nchini kote.

Lembeli akiwa na furaha, tofauti na siku nyingine, aliushangaza umati uliokuwa katika ukumbi huo, akiwamo Mkuu wa Wilaya hiyo, Benson Mpesya. 

“Nakupongeza sana ndugu yangu Mgeja, chama kimekuamini na kuthamini utendaji wako na uaminifu wako na hali hii ndiyo iliyopelekea kuteuliwa kwako ili uitetee nafasi yako ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga.

“Mimi mwenyewe nimeridhika kwa jina langu kutorudishwa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kugombea nafasi hii. Natamka wazi, sina kinyongo ninayaheshimu maamuzi ya chama,” alisema.

Kwa upande wake, Mgeja alimshukuru Mungu na kuipongeza NEC iliyokaa hivi karibuni mjini Dodoma chini ya Rais Jakaya Kikwete na kupitisha jina lake ili aweze kuitetea nafasi yake.

Mgeja aliwapongeza wagombea nafasi mbalimbali waliojitokeza kwa wingi kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika mkoa huo na kusema kuwa wagombea wote waliopitishwa na wale ambao hawakupata nafasi hizo wote ni sawa na hakuna aliye bora zaidi ya mwenzake. 

“Nafasi zilikuwa ni chache, nawaomba msikate tamaa, kipindi hiki tunahitaji upendo, umoja na mshikamano wa dhati ndani ya chama,” alisema.

Mgeja pia alimpongeza Lembeli kwa kuonyesha uzalendo na kutanguliza maslahi ya chama mbele kwa kukubali uamuzi uliotolewa na vikao vya chama ngazi ya Taifa.

“Kitendo alichofanya Lembeli ni kitendo cha uungwana na kinafaa kuigwa na wanachama mbalimbali nchini, hasa wanaokitakia mema Chama Cha Mapinduzi,” alisema Mgeja.

Chanzo: Mtanzania

0 comments:

 
Supported by Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa