Home » » MWANAHARAKATI AWALILIA WALEMAVU WA NGOZI

MWANAHARAKATI AWALILIA WALEMAVU WA NGOZI


Na Editha Edward, Shinyanga

WAZAZI na walezi wenye watoto ambao niwalemavu wa ngozi (albino), wametakiwa kuachana na tabia ya kuwatelekeza watoto hao katika vituo maalumu vya kulelea watoto.

Hali hiyo imewafanya baadhi ya watoto hao kutofahamika wanaishi maeneo gani na mahali walipozaliwa na kwamba, wakati wa likizo watoto hao huendelea kubaki vituoni.

Hayo yalielezwa jana na Mwanaharakati Josephat Torner, anayetetea masuala ya walemavu wa ngozi nchini katika Kituo cha Buhangija wilayani Shinyanga.

Torner alikuwa akikabidhi msaada wa magodoro 20 yenye thamani ya zaidi ya Sh milioni moja, kwa kituo hicho kinacholelea watoto wenye ulemavu wa aina mbalimbali. 

“Mtoto akizaliwa anakimbizwa shule maalumu kisha wazazi wao wanaendelea na maisha bila ya kuja kuwajulia hali watoto wao, huku wakidiriki kuhama maeneo.

“Inasikitisha mtoto kutomjua mama yake na wala kufahamu sehemu aliyozaliwa hata wakati wa likizo wanaendelea kuishi kituoni kwa imani akirudi katika familia atauwawa,” alisema. 

“Kwa sasa suala hili limekuwa janga la kitaifa kwa sababu kila mkoa hali hii ipo. Huu ni wakati wa kujiuliza kwa nini litokee sasa na sio zamani?,” alihoji.

Alisema, tangu kuanza kwa mauaji ya walemavu wa ngozi mwaka 2007 taifa limepata doa kubwa, kwa watu wenye ulemavu huo ambapo takribani watu 72 walipoteza maisha na watu 28 wakijeruhiwa.

Kwa upande wake Ofisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Shinyanga, Jesca Kagunila alisema msaada huo ni mkubwa, kwani mtoto mwenye ulemavu anastahili kulala sehemu nzuri kama mtoto mwingine.

Chanzo: Mtanzania



0 comments:

 
Supported by Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa