Home » » NAUNGA MKONO ZITTO KUWANI URAIS-KIGWANGALA

NAUNGA MKONO ZITTO KUWANI URAIS-KIGWANGALA




Na Suleiman Abeid, Shinyanga 

MBUNGE wa Jimbo la Nzega mkoani Tabora, Dkt. Hamis Kigwangala, ametangaza kuunga mkono dhamira ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa tiketi ya CHADEMA, Bw. Zitto Kabwe,  ya kutangaza kuwania urais mwaka 2015.


"Naunga mkono Bw. Zitto kwa dhamira yake ya kutaka kuwania uongozi wa juu kabisa katika nchi yetu japokuwa yuko CHADEMA na mimi niko
CCM," alisema Dkt. Kigwangwala.

Dkt. Kigwangwala alitoa kauli hiyo alipokuwa akiwahutubia wanafunzi wa Sekondari ya Shinyanga, iliyopo wilayani Kishapu mkoani hapa, wakati wa mahafali ya 46. Katika mahafali hayo, Dkt. Kigwangwala alikuwa mgeni rasmi.

Mbunge huyo alisema vijana wanaomaliza masomo yao wasipokuwa na malengo ya kuwa viongozi wa nchi itakuwa hatarini kujikuta ikikosa vijana makini.

Hapo ndipo alipotolea mfano Bw. Zitto, akisema alisoma naye shule moja, ambapo tangu akiwa masomoni alikuwa na ndoto ya kuwa kiongozi.

“Binafsi nampongeza kijana mwenzagu Zitto (Kabwe), maana tangu tukiwa shuleni alikuwa na malengo ya kuwa kiongozi, sasa hivi ametangaza nia yake ya kutaka kuwania urais wa Tanzania mwaka 2015,  ameniwahi hata mimi natamani siku moja nitakuwa rais, lakini leo hii hapa sitangazi nia hiyo,” alisema Dkt. Kigwangwala na kuongeza; 

“Muda wake bado, ipo siku nitatangaza dhamira hiyo,  akijitokeza kijana nitamuunga mkono...kwa hiyo namuunga mkono Zitto kwa dhamira yake ya kutaka kuwania uongozi wa juu japo naelewa hawezi kutushinda CCM.” 

Ili taifa liendelee kupata viongozi, Dkt. Kigwangwala alisema hakuna sababu  ya vijana waliopo mashuleni kubaki na dhana kuwa masuala ya siasa yanahusu wanasiasa waliopo madarakani au watu wazima peke yake, badala yake waanze kujiwekea malengo yatakayowawezesha kushika uongozi wa nchi.

Aliwataka vijana watakaobahatika kuingia katika siasa na kupata nafasi za uongozi kujiepusha na siasa za makundi ambazo hivi sasa zinaitafuna nchi.

“Epukeni makundi yanayohujumu Serikali na hatimaye kutaka uongozi wa nchi yetu, hakikishesni mnawakwepa wanasiasa wa aina hiyo, maana hawafanyi siasa kwa malengo ya jamii, hawafanyi siasa kwa malengo ya umma wanafanya siasa kwa malengo ya kutunisha matumbo yao,"alisema Dkt. Kigwangala.
   
Kwa upande mwingine, Dkt. Kigwangala alijitolea kuichangia shule hiyo msaada wa vitanda vyenye thamani ya sh. milioni tatu, kabati mbili kwa ajili ya chumba cha wanafunzi wasioona, na vifaa mbalimbali vya michezo.

Chanzo: Majira

0 comments:

 
Supported by Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Shinyanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa